Pages

Ads 468x60px

Thursday, June 4, 2015

BREAKING NEWS: Samweli Sitta: Nina Ari, Uwezo Na Utayari Wa Kuliongoza Taifa Hili......Nipeni Hii Miaka Mitano Nifanye Mabadiliko Makubwa



WAZIRI wa Uchukuzi, Samuel Sitta ametangaza rasmi nia ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia CCM na kusema ana ari, uwezo na utayari wa kuiimarisha nchi na kwamba kipindi kimoja tu cha miaka mitano kinamtosha.
 
Mbali na hilo, Sitta amesema akifanikiwa kupata nafasi ya kuongoza nchi atahakikisha anatenganisha masuala ya siasa na biashara, kwa sababu ndiyo chanzo cha rushwa kubwa na kufikiwa kwa mikataba mibovu.
 
Alitangaza nia yake hiyo jana kwenye eneo la Itetemia (Ikulu) mkoani Tabora ambako kulikuwa na makao makuu ya mashujaa wa Unyanyembe wakiwemo Isike na Kiyungi walioendesha harakati dhidi ya dhuluma na unyanyasaji wa wakoloni.
 
Pia, neno ‘Ikulu’ asili yake ni Itetemia baada ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ilipofika mwaka 1961 kuamua kulitumia neno hilo la Kinyamwezi liwe mbadala wa maneno ya kikoloni ya ‘State House’ kwa ofisi na makazi ya mkuu wa nchi ambayo kwa sasa yapo eneo la Magogoni, Dar es Salaam.
 
“Uimara wangu kiuongozi nitajumuisha nguvu na maarifa ya wananchi ili tuvuke salama na pia tutekeleze kazi za maendeleo kwa ufanisi na tija zaidi. ...nakuja kwenu Watanzania kuomba niwatumikie katika nafasi hii ya juu ya uongozi. Ninayo ari, ninao uwezo na utayari wa kuiimarisha nchi yetu katika kipindi cha miaka mitano ijayo ya utawala,” alisema Sitta.
 
Katika hotuba yake hiyo, Sitta aliainisha baadhi ya vipaumbele na kuwa kimojawapo ni kupambana kwa nguvu zote na vitendo vya rushwa kiasi kwamba akifanikiwa kuingia madarakani atatenganisha masuala ya siasa na biashara.
 
Akifafanua kuhusu hilo, Sitta ambaye aliwahi kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alisema rushwa kubwa zimekuwa na athari mbaya kwa uchumi wa nchi yetu ambapo mikataba mibovu ya huduma na mauzo, manunuzi hewa, manunuzi yaliyojaa unyonyaji, uteuzi wa wazabuni kwa rushwa na hata rushwa katika ajira, vimesababisha hasara ya matrilioni ya fedha kwa taifa.
 
“Uchumi unakosa afya kutokana na kubanwa na rushwa ambayo sasa imeenea mijini na hata vijijini...kwa hatua ya kwanza hatuna budi kutenganisha biashara na uongozi.
 
"Mtu achague kimoja; biashara au uongozi wa siasa. Ikiwa mfanyabiashara atataka kuingia katika uongozi wa siasa itabidi akabidhi mali na biashara zake kwa mdhamini atakayeendesha biashara hizo wakati mhusika anatumikia Umma,” alisema Sitta.
 
Aliongeza kuwa kwa sasa baadhi ya wanasiasa na watumishi waandamizi serikalini wanatumia nafasi zao kujitajirisha kupitia kujipendelea na kuwa jambo hilo lina athari zake ikiwemo; kuchochea rushwa na usumbufu kwa wananchi; kupunguza ari ya wafanyabiashara wa dhati na kudumaza uwekezaji.
 
Sitta alitaja hatua nyingine katika kukabiliana na rushwa kuwa ni kutunga sheria mpya zilizo kali na ambazo zitakuwa na matokeo ya kumzuia mtu asitamani kusaka rushwa, mali za viongozi zitamkwe kwa uwazi, mali isiyolingana na kipato na kukosa maelezo ya kutosheleza itaifishwe, kesi za rushwa ziwe na utaratibu wenye uwazi na tume inayoshughulikia maadili ya viongozi ipewe nguvu kubwa za uchunguzi na ufuatiliaji wa mali za viongozi bila kuzuiwa na mamlaka yeyote.
 
“Sambamba na kupiga vita rushwa, hatuna budi kuchukua hatua kali dhidi ya hujuma za uporaji wa maliasili za nchi na rasilimali zake.
 
"Madini, misitu, vyanzo vya maji, bahari, maziwa namito ni rasilimali ambazo zisipotunzwa zitatishia uendelevu wa uchumi kwa vizazi vijavyo, kwa hivyo uhalifu dhidi ya maliasili na rasilimali za nchi itabidi uwekewe sheria na taratibu kali,” alionya Sitta.
 
Akieleza kuhusu vipaumbele vyake vingine, Sitta alisema kwa maoni yake kipindi cha miaka mitano ijayo kina mwelekeo wa mifarakano katika masuala ya Muungano, kutetereka kwa mshikamano kunakotokana na chokochoko za siasa za ushindani, udini na kupanuka kwa tofauti ya kipato na ongezeko la kundi kubwa hususani la vijana mijini lisilo na uhakika wa ajira.
 
Kutokana na hali hiyo, alisema atatumia mchanganyiko wa uzoefu wa uongozi kutanzua changamoto hizo ikiwemo ya Muungano. Kuhusu hilo la Muungano alisema kwa sasa zinajitokeza kauli na vitendo ambavyo vinaashiria kutaka nchi mbili zilizoungana zitengane.
 
“Kutoka Zanzibar, tunashuhudia wanasiasa wanaodai kuwa Zanzibar itanufaika zaidi ikirejea kuwa na uhuru kamili bila kuwa ni sehemu ya Muungano.
 
"Baadhi ya wabara nao wanawatazama ndugu zao wa Zanzibar kuwa ni wakorofi wasioridhika na chochote kitakachofanywa na Muungano na wanahisi kuwa mfumo wa Muungano uliopo unaipendelea Zanzibar ili hali baadhi ya Wazanzibari nao wanadai kuwa Bara inapendelewa.”
 
Sitta alijinadi kuwa kiongozi anayeweza kuzileta pamoja kambi hizi na kuuokoa Muungano hana budi kuwa na ufahamu mzuri wa kutosha wa asili, misingi na manufaa ya Muungano.
 
“Ushiriki wangu katika serikali yetu tangu awamu ya kwanza ya uongozi wa nchi yetu unaniweka katika nafasi nzuri ya kuongoza mchakato utakaowezesha kuzijadili na kuzipatia ufumbuzi changamoto za Muungano.”
 
Kipaumbele kingine alitaja ni kuhusu mchakato wa Katiba ambapo alisema licha ya mwafaka kamili kuhusu katiba mpya kutofikiwa, lakini Katiba Inayopendekezwa ina maeneo mengi ya msingi ambayo yanaweza kutuleta karibu ikiwa ni hatua ya awali inayowezesha kusonga mbele kwa amani.
 
Jingine atakalolipa kipaumbele ni kujenga mfumo wenye motisha kwa wote ili kuchochea uchumi endelevu na wa viwanda kukuza uchumi wa nchi kwa kasi inayopunguza umasikini kwa haraka.
 
Aliongeza kuwa wafanyabiashara wakubwa wa ndani hawawekezi vya kutosha ndani ya nchi ili kuleta maendeleo ya haraka ya huduma, viwanda, kilimo na biashara na kuwa baadhi yao baada ya kuchuma fedha wanazihamishia nje ya nchi huku watendaji serikalini wakiwatazama wafanyabiashara hawa kuwa hawana uzalendo na ni wakwepa kodi na wana mazoea ya kutoa rushwa.
 
Sitta anakuwa mwanasiasa wa kumi kutangaza nia ya kuwania urais huku baadhi yao wameshachukua fomu za kuwania urais kwa tiketi ya CCM.
 
Waliotangaza nia na kuchukua fomu ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Waziri wa Kilimo, Chakula la Ushirika, Stephen Wassira, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Afrika Mashariki, Charles Makongoro Nyerere na mwanadiplomasia mkongwe ambaye kwa sasa ni Balozi wa Umoja wa Afrika (AU) katika Marekani, Amina Salum Ali.
 
Wengine waliotangaza nia ni Balozi mstaafu, Ali Karume, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk Titus Kamani, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu na Mbunge wa Nzega, Dk Hamisi Kigwangallah.

0 comments:

Post a Comment

SHARE