Mio za kuwania kumrithi Rais Jakaya Kikwete miongoni mwa makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) zimezidi kushika kasi, safari hii Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, akinusurika kifo baada ya ndege aliyokuwa akisafiria kuwapo katika hatari ya kugongwa na ndege nyingine angani alipokuwa akielekea Zanzibar.
Waziri Membe akiwa na ujumbe wake wa watu nane walikuwa wakisafiria 
ndege ya kukodi kampuni ya 5H NEG Precision Aviation ikirushwa na rubani
 Mathew Mhahiki ambaye ameonesha kushangazwa na tukio hilo alilodai “ni 
kwa rehema za Mungu tumepona ajali hii.” 
Akizungumza na mwandishi wetu, rubani Mathew Mhahiki alisema, “…lazima 
kuna tatizo katika control center hata hivyo tayari nimeongea nao na 
wameniomba samahani na kudai walipitiwa maana kwa hali ilivyokuwa ni 
kwamba tungegongana wakati wa kutua, nimeshangaa tu kuona ndege hii hapa
 ndio maana nikaamua kumkwepa mwenzangu nikapanda juu.” 
Aidha, Waziri Membe aliyeonekana kushitushwa na hali hiyo alisema, 
“…nina uzoefu mkubwa wa kusafiri na ndege mahali pengi duniani, hali hii
 ilikuwa ni ajali na labda sasa tungekuwa dead bodies lakini ninajua 
Mungu yuko upande wetu katika safari hii ya uhakika, lakini pia 
izingatiwe nimekuja kufanya kazi ya Mungu.” 
“Katika safari hii tutashuhudia mambo mengi sana lakini kwa kuwa kila 
ninapotaka kuondoka nyumbani ama hotelini mara nyingi nimekuwa 
nikimtanguliza Mungu maana bila Mungu, hii ilikuwa ni mwisho wa maisha 
yetu tuliokuwa kwenye ndege hii,” alisema Membe 
Naye mwanasiasa anayenyemelea Ubunge Jimbo la Rungwe Mashariki, Richard
 Kasesela, aliyeongozana na Waziri Membe alionesha wasiwasi wa hali hiyo
 kuwa inaweza kuwa ni hujuma dhidi ya Membe.
“Katika hali ya kawaida watu wa control center hawawezi kuruhusu ndege 
mbili kutua kwa wakati mmoja maana tafsiri yake ni kuwa mtagongana na 
ndio maana kuna haja ya kujua ni kwa nini hali hii imetokea katika 
kipindi hiki cha Waziri Membe na wanasiasa wengine wanapotafuta kuungwa 
mkono kugombea nafasi ya urais kupitia Chama Cha Mapinduzi,” alisema 
Kasesela 
Taarifa nyingine kuhusu tukio hilo zinabainisha kuwapo kwa uzembe 
katika chumba cha kuongozea ndege ambapo mmoja wa wafanyakazi katika 
chumba hicho alithibitisha uzembe huo. 
“Mimi si msemaji wa ofisi yetu lakini hata sisi tumeshangazwa na hali 
hiyo maana si jambo la kawaida kutokea kama hakuna tatizo. Wengine 
tayari tulishika vichwa maana uzoefu unaonesha kuwa ukiruhusu ndege mbili 
kutua kwa wakati mmoja ni wazi unataka kusababisha ajali,” alisema kwa 
sharti la hifadhi ya jina. 
Waziri Membe alikuwa amealikwa mjini Zanzibar na Umoja wa Kinamama wa 
Kikristu (UMAKI) wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Zanzibar, waliokuwa 
wakifanya mkutano wao mkuu unaofanyika kila baada ya miaka mitano 
akitokea Iringa ambako alikwenda kutafuta wadhamini ili kumwezesha 
kugombea urais kupitia CCM. 
Akiwa uwanjani hapa Waziri Membe alikutana na Naibu Waziri wa Fedha, 
Mwigulu Nchemba aliyekuja  Zanzibar kutafuta wadhamini ambapo makada hao
 walipata nafasi ya kuzungumza na kujadiliana masuala ya siasa ndani ya 
chama chao. 
Akiwa katika mkutano wa kinamama hao, Membe alisema; “Miongoni mwa 
mambo yanayonikera ndani ya nafsi yangu ni kuona mwanamke bado anaachwa 
nyuma, hili halipendezi ni lazima tuhakikishe wanawake wanapata elimu ya
 ufundi stadi maana mwanamke akiwezeshwa hasa katika eneo hili la ujuzi,
 wanaweza hata kushinda wanaume wengi.” 
“Ni lazima kina mama wawezeshwe kujiajiri ili msiwategemee kina baba 
kwa kila jambo lakini pia ili kufikia malengo hayo ni lazima tuwape 
elimu kina mama.” 
Kina mama hao pamoja na mambo mengine wameonesha miradi mbalimbali 
wanayoifanya ikiwa ni pamoja na utengenezaji wa bidhaa mbalimbali kama 
mishumaa, asali iliyosindikwa, vitenge, siagi na bidhaa mbalimbali za 
nyumbani. 
Membe ameahidi kuwasaidia kumpata mfadhili wa kujenga kituo cha umoja 
huo na hasa jengo la utawala huku akisisitiza umoja huo pamoja na mambo 
mengine, kujenga kituo cha watoto yatima pamoja na mradi wa maji. 
Awali, akiwa mkoani Iringa Membe alisema; “Hebu wapimeni hao wanaokuja 
kwenu kwa fedha kutaka kuwanunua ili kuwaunga mkono, ni hatari maana 
kama kiongozi utajisikiaje kumtumikia mtu ambaye tayari ulimnunua kwa 
fedha” 
Aliwataka wananchi kupokea fedha wanazopewa na baadhi ya wanasiasa wanaowania urais lakini akisisitiza wawe na msimamo. 
“Hizo ni fedha zenu zichukueni mle lakini muwe na msimamo wa 
kutomchagua mtu wa namna hiyo maana hatoweza kuwatumikia maana atakuwa 
na haya,” alisema Membe 
Akizungumzia vipaumbele vyake endapo atachaguliwa kuwa mgombea urais na
 hatimaye Rais wa Tano wa Tanzania, Waziri Membe alisema atahakikisha 
nchi inapiga hatua za maendeleo kwa haraka kupitia uchumi wa viwanda 
vinavyotegemea kilimo. 
“Badala ya kuuza pamba sasa tuuze nguo, badala ya kuuza ngozi sasa 
tuuze viatu na kadhalika, uchumi wa namna hii unaweza kutoa ajira kubwa 
sana na hasa baada ya kugundulika kwa gesi asilia itakayotusaidia 
kuondokana na tatizo la nishati ya umeme,” alisema 


 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment