Pages

Ads 468x60px

Monday, June 1, 2015

Urais 2015: Kigwangalla aja na kipaumbele cha ajira .....Hapa Anaeleza Ni Kwa Nini Amechagua kuzalisha Ajira kuwa Kipaumbele cha Kwanza



Nchi yoyote ili iendelee lazima watu wake wawe na amani, uhuru, furaha, uzalendo, uwajibikaji, nidhamu ya kazi, ubunifu na uchapakazi. Ili watu wetu wawe na vitu hivi lazima tujenge misingi ya usawa na motisha. 
 
Usawa utawafanya watu waone nchi yao inawajali na hivyo watavumilia jua na mvua. Motisha itawafanya watu wawe tayari kupigania na kuifia jamii na nchi yao.
 
Motisha itawafanya watu wafanye kazi kwa bidii na maarifa bila kuchoka na hatimaye nchi itasonga mbele kwa kasi. Nchi ya namna hii itasonga mbele kwa umoja na kwa pamoja.

Kama watu maskini wakisomesha watoto kwa shida na kwa bidii halafu baada ya kuhitimu, watoto wakakosa ajira, watoto wenyewe, familia na jamii yote inakata tamaa. 
 
Kama wazazi wakishiriki kujenga shule, wakajibana wakatoa michango yao na ada ili watoto wao wasome wakitumaini watapata elimu na baadaye watawakomboa – mwishowe watoto wakakosa ajira, watakata tamaa.

Muhula unaoisha umejenga mashule ya kutosha na vyuo vikuu vya kumwaga. Kutoka sekondari 1500 mpaka zaidi ya 4500 si kazi rahisi. 
 
Kutoka walimu karibu 10,000 mpaka zaidi ya 80,000 si kazi bure. Kutoka wahitimu around 20,000 wa vyuo vikuu na vya kati mpaka takriban 100,000 ni mafanikio makubwa. Lakini wakihitimu wanaenda wapi?
 
Na wale wa sekondari nao wakihitimu na wakifeli wanaenda wapi? Maana, tunaingiza takriban vijana milioni moja kila mwaka kwenye soko la ajira, wakati tunazalisha ajira takriban 50,000 tu.

Je, tumewekeza vya kutosha kwenye ajira? Kwa wastani, bajeti ya kukuza ajira Tanzania ni asilimia 0.01 ya bajeti yote. Hiki ni kiasi kidogo sana kulinganisha na mahitaji niliyobainisha hapo juu.

Fikra zangu ni kuwa ili tufanikiwe kwenye azma yetu ya kupambana na umaskini, ujinga na maradhi, na tufikie malengo yetu ya kuleta furaha, uhuru wa kweli, amani ya kudumu na maisha bora kwa kila mtanzania ni lazima tuzalishe ajira zenye tija na ufanisi kwa kila mtanzania. 
 
Watanzania ni wachapakazi na wako tayari kuajiriwa na kujiajiri, je tumewawezesha kufanikisha haya? Tunahitaji kuwekeza kwenye kuzalisha ajira zisizo rasmi kwa wingi zaidi; tunahitaji kuwekeza kwenye kilimo na kukifanya kiwe cha kibiashara na chenye linkage na viwanda, ili mwisho wa siku tupate kodi ambayo itatumika kutoa huduma bora zaidi za afya, elimu, maji, mikopo ya nyumba za bei nafuu vijijini na mijini, na kujenga miundo mbinu (wakati huo huo tukizalisha ajira kutokana na uwekezaji huu).

Dhima ya ‪#‎KilimoKwanza imefanikiwa kutupatia uhakika wa chakula kwa miaka mitatu zaidi mbele. Awamu inayofuata ijikite kwenye ku-link uzalishaji mashambani na masoko na viwanda – kwa value addition. 
 
Elimu ndiyo, lakini siyo kipaumbele cha kwanza, na siyo elimu ya kitaaluma, zaidi iwe ya kujenga ujuzi na kuandaa wazalishaji zaidi ya maafisa, maana kusomesha watoto bila kuwajengea mazingira ya ajira ni kutengeza bomu litakalohatarisha amani na utulivu wa nchi yetu.
 
 Tuwatajirishe watu kisha watasoma na kusomesha. Ni mzazi gani atahangaikia mahitaji ya shule ya mtoto kama hana chakula cha kumlisha?

Ni lazima tuwekeze kwenye mfumo wa kisasa na shirikishi wa mikopo kwa wakulima na wafanyabiashara za kati na ndogo ndogo ili wazalishe bidhaa kwa ajili ya viwanda vya kati na vikubwa.
 
 Ni lazima kilimo chetu kiwe commercialised na kiwe linked na manufacturing – no short-cut. Hii itapunguza uagizaji wa bidhaa nyingi kutoka nje na kusaidia kutunza akiba ya fedha zetu za kigeni. Uzalishaji huu utaleta kodi zaidi. 
 
Ni lazima tuwekeze kwenye miradi mikubwa ya gesi, uchimbaji madini na ujenzi ili kuzalisha ajira kwa watu wetu. Kila mtu akiwa na ajira tutajenga Taifa la watu wenye furaha na uzalendo kwa nchi yao.
 
 Uwekezaji kwenye sekta hizi utahitaji wasomi, ndiyo, lakini kipi kinaanza kwanza, kwa hapa tulipo? Kuwekeza kwenye elimu zaidi ama kwenye kuzalisha ajira kwa kukuza uchumi na kuondoa umaskini?

Leo hii ukitaka, na hata kama unatamani kuzalisha wasomi zaidi hauwezi kufanikiwa maana hauna pesa za kufanya hivyo. Hata ukitamani kujenga hospitali na zahanati zaidi na kupeleka madawa na wataalamu zaidi hautoweza sababu hauna hela (wishful thinking tu). 
 
Ni lazima uwe na pesa kwanza ndipo ufanye haya mengine. Ndiyo maana ninaamini, pamoja na umuhimu wa elimu, afya na maji, ni lazima uwekeze kwenye kukuza uchumi kwanza ndipo ufanye haya. 
 
Hivyo nimeweka kipaumbele cha kwanza kwenye kutatua changamoto ya ajira nchini, na cha pili kutoa huduma bora za kijamii. Changamoto ya ajira nchini suluhu yake ni kukuza uchumi tu hakuna namna nyingine. ‪#‎AjiraKwanza.

Hata hivyo la muhimu zaidi si kuibuka na slogan kila kukicha, ni kutenda. Watanzania wanahitaji kuona mambo yakifanyika na wakishirikishwa kufanya mambo, siyo kuimbiwa nyimbo nzuri za matumaini hewa.

0 comments:

Post a Comment

SHARE