Pages

Ads 468x60px

Sunday, June 7, 2015

Mangula amsafishia njia Msambatavangu>>>>SOMA HAPA



MWENYEKITI wa CCM Mkoa wa Iringa, Jesca Msambatavangu, amesema anayo nia na uwezo wa kumwangusha Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa (Chadema) katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba.
 
Kauli hiyo aliitoa mjini hapa jana ikiwa ni siku tatu baada ya Makamu Mwenyekiti wa CCM (Tanzania Bara), Phillip Mangula, kumaliza mgogoro wa kisiasa uliosababisha baadhi ya wanachama wa chama hicho Iringa Mjini wafukuzwe uanachama huku Msambatavangu akipewa onyo kali.
 
Machi mwaka huu, vikao vya chama hicho ngazi ya wilaya na mkoa viliwafukuza uanachama Shukuru Luhambati, Clara Shirima na Hosea Kaberege huku Msambatavangu akipewa onyo kali lililodaiwa kumwondolea sifa ya kugombea nafasi yoyote ya uongozi kupitia chama hicho na kuzusha hofu ya mpasuko.
 
Akizungumzia rufaa walizokata na uamuzi aliokuja nao Mangula na kuwasilisha katika kikao cha Halmashauri ya Manispaa ya Iringa, alisema: 
 
“CCM kwa kutumia kanuni na katiba yake imepitia rufaa zetu, ikajifunza kitu na kutumia busara yake kutupilia mbali adhabu hizo ili kulinda masilahi mapana ya chama hiki.
 
“Tunajiandaa kushiriki Uchaguzi Mkuu tukiwa wamoja na niwahakishieni mimi ni mmoja kati ya wana CCM wenye nia ya kugombea ubunge katika Jimbo la Iringa Mjini.
 
“Sijajua makada gani wengine watajitokeza wenye uwezo wa kusema ni nani, ni CCM wenyewe na wananchi wa jimbo hili.
 
 “Kwa mimi kutangaza nia na kujitoa nina hakika na ninafahamu nina uwezo wa kupeperusha bendera na kurudi na ushindi, sitailetea aibu CCM na nipo tayari kumuunga mkono mgombea atakayeteuliwa.”
 
Alitaja kipaumbele chake cha kwanza endapo CCM itampa ridhaa ya kuwania nafasi hiyo kuwa ni elimu na katika sekta hiyo atakahikisha miundombinu yake inaboreshwa ili iwe ya kisasa.
 
Alisema katika kuboresha ustawi wa elimu, atahakikisha vijana wengi wa shule za msingi na sekondari za Iringa Mjini wananufaika kwa uwapo wa vyuo vikuu vinne vya mjini hapa kwa kutengeneza ushirikiano utakaosaidia vijana wengi kujiunga na elimu ya juu.
 
Msambatavangu alisema licha ya CCM kuwa wapinzani katika jimbo hilo, lakini bado wana nguvu ya kutosha kisiasa na ndiyo maana walipata viti vingi katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
 
Katika uchaguzi huo, CCM ilipata viti 126, Chadema 64 na CUF kimoja.
 
Kama atatimiza azma yake hiyo, Msambatavangu ambaye ni msomi mwenye Shahada ya Uzamili ya Usimamizi wa Biashara atakuwa anaingia kwa mara ya pili katika kinyang’anyiro hicho.
 
Katika kura za maoni ndani ya CCM zilizoshirikisha wagombea 12 mwaka 2010, alikuwa mtu wa nne baada ya kupata kura 916 nyuma ya Frederick Mwakalebela aliyepata 3,897, Monica Mbega 2,989 na Dk. Yahaya Msigwa 1,217.

0 comments:

Post a Comment

SHARE