BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Watanzania limewasimamisha wabunge 11 kwa kudharau mamlaka ya Spika jana.
Hatua hiyo ni baada Spika wa Bunge hilo, Anne Makinda, kuwashitaki 
katika Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, 
wabunge hao wa Kambi Rasmi ya Upinzani, wakiongozwa na Mnadhimu Mkuu wa 
Kambi hiyo, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema).
Makinda alichukua hatua hiyo, baada ya wabunge hao kurudia kwa mara 
ya pili kufanya vurugu na kupiga kelele wakati kikao kikiendelea na 
kumlazimisha kuahirisha kwa mara ya nyingine shughuli za bunge 
zilizokuwa zikiendelea bungeni mjini hapa.
“Bunge haliwezi kuendeshwa kwa kelele na vurugu namna hii. Kwa mujibu
 wa Kanuni za Bunge, ninawataja kwa majina vinara wa vurugu ambao 
walitakiwa kufika kwenye Kamati ya Maadili na kulazimika kuahirisha 
Bunge hilo hadi jioni."
Hukumu ya Watuhumiwa
Kamati hiyo ilitoa adhabu kwa mafungu matatu ambapo wapo ambao 
hawakutoa ushirikiano kabisa kwa kamati hiyo wakidai wangefanywa hivyo 
mbele ya wanasheria wao, hao walifungiwa moja kwa moja, waliotoa 
ushirikiano kwa kamati wakafungiwa kutohudhuria vikao viwili na wengine 
waliochelewa kupata wito wanatakiwa kuhojiwa na kama leo asubuhi saa nne
 wakati mmoja hakuguswa na adhabu hizo kabisa.
Waliosimamishwa moja kwa moja ni Lissu, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika
 (Chadema), Mbunge wa Viti Maalumu, Paulina Gekul (Chadema), Mbunge wa 
Mohambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Kasulu Mjini na 
Moses Machali (NCCR-Mageuzi).
Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema), Rashid Ally Abdallah 
(CUF) na Mbunge wa Gando, Khalifa Khalifa (CUF), hao wanatakiwa kufika 
katika kamati hiyo ya maadili leo kwa kuwa hawakupata wito wa kuitwa 
jana mapema huku Mbunge David Silinde hakuguswa kabisa katika adhabu 
hiyo.
Kundi la pili waliofungiwa vikao viwili, cha leo na Jumatatu ni 
Mbunge wa Ole, Rajab Mbaruk Mohamed (CUF) na Mbunge wa Iringa Mjini, 
Peter Msigwa (Chadema) ambao waliitikia wito na walitoa ushirikiano kwa 
Kamati hiyo ambayo Makamu Mwenyekiti wake ni Brigedia Hassan Ngwilizi, 
ambaye ni Mbunge wa Mlalo (CCM).
Akiwasilisha maamuzi ya kamati hiyo, Mwenyekiti wa kamati alisema 
walifikia maamuzi hayo baada ya kuridhika baada ya kuwaita wahusika na 
kujieleza na hatimaye kufikia maamuzi hayo.
Kamati hiyo ambayo Makamu Mwenyekiti wake ni Kapteni John Chiligati, 
ambaye ni Mbunge wa Manyoni Mashariki (CCM) ilitoa maamuzi hayo 
kulingana kanuni za Bunge.
Ilivyokuwa
Vurugu hizo zilianza mara baada ya Lissu kusimama kuomba Mwongozo wa 
Spika, wakati Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene alipokuwa
 akisoma kwa mara ya pili, muswada wa Sheria ya Mafuta na Gesi wa mwaka 
2015, ambao Kambi ya Upinzani ilikuwa ikiupinga tangu mwanzo.
Wakati wakipiga kelele, Spika alinyamaza na Simbachawene akaendelea 
kusoma muswada huo, ndipo wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani wote 
waliokuwepo bungeni wakasimama kumuunga mkono Lissu na kuwalazimu baadhi
 ya wabunge wa CCM kuanza kuwazomea na wao kurudisha maneno 
yaliyosababisha hata aliyekuwa akisoma asisikike.
Msimamo wa upinzani
Pamoja na yaliyotokea, kambi hiyo ilijikusanya ndani ya Bunge hilo 
kupeana misimamo ambapo, walisikika wakisema hata iweje, hawatakubali 
muswada huo wa Sheria ya Mafuta na Gesi upite.
Katika hatua nyingine, Spika Makinda alikataa kuendekeza malalamiko 
ya Mbunge wa Viti Maalum, Martha Mlata (CCM), aliyeomba mwongozo na 
kudai kuwa, Mbunge wa NCCRMageuzi, Moses Machali alimdhalilisha kwa 
kumwambia kuwa, alifumaniwa na wajinga wenzake.
Machali alisema hivyo alipokuwa akitoa maoni ya muswada uliopitishwa 
wa Ulinzi wa Mtoa Taarifa za Uhalifu na Mashahidi, baada ya kukasirishwa
 na kitendo cha Mlata kuropoka kuwa Mbunge huyo aliyetaka adhabu iwe 
kunyongwa ni kichaa.
“Leo wote mmeonesha utovu wa nidhamu wa hali ya juu, kwa kutoleana 
maneno yasiyofaa. Wengine mmekuwa mkiingilia hoja za wenzenu wakati 
wanaziwasilisha, kwa kuwatolea maneno yasiyo na adabu,” alisema.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment