Pages

Ads 468x60px

Monday, June 1, 2015

January Makamba: Taifa liko njia panda, Wananchi Chagueni Kiongozi Atakayeleta Maendeleo



NAIBU Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba, amesema kwa sasa nchi ipo njia panda, hivyo kuna haja ya kutumia busara ili kuchagua kiongozi atakayeleta maendeleo.
 
Kauli hiyo aliitoa Dar es Salaam mwishoni mwa wiki , wakati akizungumza na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Tumaini Tawi la Mwenge, kuhusu utandawazi na maendeleo ya jamii.
 
January, Mbunge wa Bumbuli, ambaye pia ametangaza kutaka kugombea urais, alisema Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba, mwaka huu ni muhimu kuliko zote, kutokana na wananchi kuwa njia panda ambayo moja ina mashimo na nyingine ina mafanikio.
 
Alisema matamko mbalimbali ya viongozi wa dini katika sherehe za sikukuu na mwaka mpya yanaonyesha nchi ipo njia panda kutokana na wananchi kukosa amani ya moyo.

“Uchaguzi huu una majaribu mengi, kuna viongozi wanafanya kazi ya kutoleana lugha kali na kushutumiana wizi, tafadhali angalieni uchaguzi huu ni muhimu na tunaweza tukachagua watu watakatuingiza shimoni ama watakaoweza kutupeleka katika mafanikio,” alisema January.
 
Alisema hiki ni kipindi cha tatu ambacho Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinaingia katika uchaguzi wa ndani, hivyo anaamini bado kinaendelea kujifunza katika masuala hayo.
 
Alisema kuna mambo yanaonyesha wazi kuwa katika kipindi hiki nchi inajaribiwa,  hivyo busara za viongozi zinahitajika ili kuweza kuivusha nchi salama na watu waishi vizuri baada ya uchaguzi.
 
Alisema vijana pia wana nafasi kubwa ya kupaza sauti ili kupata viongozi bora, ikiwa pamoja na kuuliza maswali kuhusu hatima ya nchi badala ya kushabikia.
 
Mmoja wa wanafunzi alimuuliza endapo atakuwa rais atafanya nini ili Ikulu isiwe pango la walanguzi, lakini alijibu hawezi kuongelea masuala ya siasa katika eneo la taaluma.
 
“Nisingependa katika mazungumzo haya kusema nitafanya nini nikichaguliwa ili mnichague, swali linaloelekeza huko sitojibu, tusifanye siasa kwa sababu hii ni sehemu ya taaluma, kama unataka mambo hayo nitafute mtaani au katika mitandao,” alisema January.
 
Pia aliitaka Tume ya Uchaguzi (NEC) kuharakisha mchakato wa uandikishaji wapiga kura ili kuhakikisha watu wanapata haki ya kupiga kura.
 
Alisema hatafurahi kuona mtu anashindwa kupiga kura kwa sababu za kutojiandikisha, badala yake asiyepiga kura awe ni kwa sababu zake binafsi.

0 comments:

Post a Comment

SHARE