Pages

Ads 468x60px

Sunday, June 7, 2015

BREAKING NEWS>> Midahalo Watangaza Nia CCM Ruksa......Kinana Asema Nafasi Wanayoomba ni Kubwa, Ataka Wahojiwe wananchi Wawasikie



SIKU moja baada ya Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Mohamed Seif Khatib kupiga marufuku pamoja na mambo mengine makada wa chama hicho waliochukua fomu kuwania urais kushiriki midahalo, Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana amepinga msimamo huo.
 
Badala yake, Kinana ameruhusu makada hao wanaoomba ridhaa ya kupeperusha bendera ya chama hicho kwa nafasi ya urais kushiriki katika midahalo iliyoandaliwa na Umoja wa Watendaji wa Kampuni binafsi (Ceo's roundtable), huku akiwataka waandaaji wa midahalo hiyo kutenda haki ili kuepusha mifarakano.
 
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Bukoba jana, Kinana alisema midahalo hiyo inaweza kuwafanya wananchi kuwatambua wagombea wao na kuwapima kwa hoja kama wanaweza kuongoza nchi au la ili waweze kuwapigia kura.
 
“Nimepigiwa simu na baadhi ya wagombea waliotangaza nia ya kuwania nafasi ya urais ndani ya chama, sasa nawaambia kuwa wana hiari ya kwenda au kutokwenda kwa sababu ni uamuzi wao binafsi na si suala la chama.
 
“Wakati walipotangaza nia na kuchukua fomu walisema mengi sana ikiwamo jinsi watakavyoweza kuongoza nchi na wananchi wamewasikia, hivyo basi chama hakina uwezo wa kuwakataza kushiriki kwenye midahalo hiyo,” alisema.
 
Juzi Seif Khatib alikaririwa na vyombo vya habari akisema hakuna mgombea urais yeyote atakayeruhusiwa kushiriki midahalo hiyo hadi hapo chama kitakapompata mgombea mmoja wa nafasi hiyo.
 
Hata hivyo Kinana jana aliwaambia waandishi kuwa mdahalo huo si wa CCM, bali umeandaliwa na watendaji wengine ili kuwapima wagombea hao katika kipindi hiki wanachotaka kuwania nafasi ya uongozi.
 
Alisema haoni haja ya chama kuwakataza kushiriki katika midahalo hiyo wakati nafasi wanazozitaka ni za kitaifa na kimataifa ambazo zinawahusisha wananchi wenyewe, hivyo wanapaswa kushiriki ili waweze kupimwa.
 
“Chama hakiwezi kuwazuia watangaza nia kushiriki kwenye midahalo kwa sababu nafasi wanazoomba ni za kuwatumikia wananchi, kama kuna mdahalo ambao utawafanya kujibu hoja na kutoa ufafanuzi, wanachama wa CCM watawapima hoja zao na wananchi watawapima zaidi ili waweze kujua nani anayewafaa,” alisema.
 
Alisema kutokana na hali hiyo, walioandaa midahalo hiyo wanapaswa kutenda haki na si kuwabeba watangaza nia, jambo ambalo linaweza kuleta mifarakano isiyo na sababu.
 
“Lengo la midahalo iwe ni kuwasaidia wananchi kuwafahamu wagombea wao ili waweze kufanya uamuzi sahihi,” alisema.
 
Alisema kutokana na hali hiyo waandaaji wanapaswa kuangalia masilahi ya wananchi  ili waweze kujua sera zao na kujenga hoja ambazo zitawasaidia kuwapima.
 
Kinana alisema midahalo hiyo isijenge chuki na kuleta mifarakano ambayo itawafanya wagombea kugombana, jambo ambalo linaweza kusababisha mifarakano.

0 comments:

Post a Comment

SHARE