Pages

Ads 468x60px

Wednesday, June 10, 2015

Amina Salum: Tanzania Inahitaji Rais Mwanamke



MGOMBEA Urais wa Tanzania ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Amina Salum Ali amesema wanawake hawana sifa ya ufisadi na ufujaji wa mali za umma na kwamba Tanzania inahitaji Rais Mwanamke.
 
Akizungumza na waandishi wa habari pembezoni mwa uwanja wa ndege wa Karume kisiwani Pemba, Balozi Amina alisema kwamba wanawake ni watu wanaaminifu wanaojali dhamana zao.
 
“Wanawake sio wafujaji, ni watu waaminifu ambao wanajali dhamana walizopewa na ni walezi wazuri” alisema Balozi Amina.
 
Balozi Amina alisema kwamba kazi ya Urais, inahitaji mtu mwadilifu, mchakapazi mbali ya sifa nyingine, ambazo kama Tanzania itaongozwa na Rais mwanamke itasonga mbele kiuchumi kwa mwendo wa haraka zaidi.
 
Alisema katika nchi ambazo viongozi wake ni wanawake, zimepata mafanikio ya kiuchumi, kisiasa na kijamii. Alitoa mfano, Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel ambaye anaiongoza Ujerumani katika uchumi imara miongoni mwa nchi za Umoja wa Ulaya (EU).
 
Balozi Amina anamtaja Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, marehemu Margaret Thatcher ambaye amejenga msingi imara wa uchumi wa Uingereza huku akimtaja pia Rais wa Brazil, Dilma Rousseff kuwa ni kiongozi mwenye mafanikio katika nchi yake.
 
Balozi Amina anamtaja pia Waziri Mkuu wa zamani wa India, Indira Gandhi kuwa naye alikuwa kiongozi hodari, shupavu na kwa uchapaji wake wa kazi, India imesonga mbele kiuchumi kwa kuweka misingi madhubuti wakati wa uongozi wake.
 
Wanasiasa wengine wanawake aliowataja ni pamoja na Waziri Mkuu wa zamani wa Pakistan, Benazir Bhutto na Rais Ellen Johnson wa Liberia ambaye amefanikiwa kutokomeza maradhi ya ebola kwa ushupavu wake.

0 comments:

Post a Comment

SHARE