Pages

Ads 468x60px

Wednesday, June 10, 2015

CCM ikisimamisha mla rushwa, itapoteza dola, asema Wassira>>SOMA HAPA



WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wassira amesema iwapo Chama Cha Mapinduzi (CCM) kitafanya kosa kumsimamisha mgombea mla rushwa, kitapoteza dola.
 
Akizungumza jana na waandishi wa habari baada ya kudhaminiwa katika ofisi za CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Wassira alisema kamwe wana CCM hawatakubali kupoteza dola, badala yake atateuliwa mtu safi.
 
Mgombea huyo alisema Watanzania hawana nchi, ambayo iko sokoni na akaongeza kuwa kama Tanzania ingekuwa inauzwa, wangetangaza zabuni ya kuinunua, hivyo akawataka wagombea wenzake wanaotumia rushwa, kuacha.
 
Alisema yeye hatoi rushwa na anatafuta wadhamini mikoani kwa kutumia gari na sio kupanda ndege au helikopita.
 
Alisema hadi jana alikuwa ameshapata wadhamini kutoka mikoa 15 na akasisitiza kuwa atazunguka nchi nzima, kusaka wadhamini kwa kutumia gari lake.
 
Hata hivyo, Wassira aliwasihi wagombea urais wa CCM ambao wametangaza nia na wale ambao wamechukua fomu kuomba kugombea urais, wasigombane kwani kufanya hivyo kutawanufaisha wapinzani.
 
Alisema ugomvi wa miongoni mwa wana CCM, uliwanufaisha wapinzani katika majimbo ya Kawe na Ubungo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, hali ambayo ilisababisha CCM kupoteza majimbo hayo kwa vile tu wagombea waliingia kwenye ugomvi.
 
“Mimi nagombea na sitaki kugombana na mtu na nawasihi wenzangu wengine pia tusiingie kwenye ugomvi kwani kufanya hivyo wapinzani watapita katikati yetu na kushinda uchaguzi,” alisema Wassira.
 
Wassira alisema ana hakika atashinda na atakipokea kijiti kutoka kwa Rais Jakaya Kikwete na akawataka wana CCM, waamua kwa haki na sio kwa rushwa.
 
 “Haki itapatikana katika mazingira tulivu na sio mazingira ya rushwa,” alisema Wassira.

0 comments:

Post a Comment

SHARE