Pages

Ads 468x60px

Monday, June 15, 2015

Bunge Latoa Ufafanuzi Kuhusu VICOBA>>soma hapa



Ofisi ya Bunge imebaini uwepo wa Waraka usiokuwa na Nambari ya Kumbukumbu wala Tarehe wenye kichwa “KUIDHINISHWA KWA MFUKO WA FOCUS VICOBA” unaosambaa kupitia njia mbalimbali ikiwemo mitandao maarufu ya Facebook na WhatsApp. Waraka huo una maneno yafuatayo:
 
“Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania linaidhinisha na kutambua uwepo wa mfuko wa utoaji mikopo FOCUS VICOBA. Viongozi wakuu wa bunge na wabunge kwa ujumla tumepitisha huduma za mikopo inayotolewa na Taasisi ya Vicoba kupitia mfuko wa FOCUS VICOBA kwa lengo la wajasiriamali kupata mikopo inayotolewa katika mfuko huu wa FOCUS VICOBA.”
 
Ofisi ya Bunge inapenda kuutaarifu umma kwamba Waraka huo siyo wa kweli na kwamba Viongozi Wakuu wa Bunge na Wabunge kwa ujumla hawajawahi kujishughulisha na hoja wala masuala ya Taasisi ya VICOBA. 
 
Aidha, Ofisi ya Bunge inapenda kuueleza umma kwamba barua na nyaraka zote za Bunge hutumia nembo ya Bunge kama inavyoonekana hapo juu na si ya Serikali. Vile vile muhuri na sahihi ya Katibu wa Bunge viliyo katika Waraka huo havifanani kabisa na muhuri na sahihi halisi ya Katibu wa Bunge. Hivyo ni dhahiri kwamba Waraka unaosambaa ni wa kutunga.
 
Wakati Ofisi ya Bunge inaendelea kufanya uchunguzi ili kujua Wahusika na kutafakari dhamira ya kutungwa na kusambazwa kwa Waraka huo na kuchukua hatua stahiki, Umma unatahadharishwa kutojihusisha na Mfuko wa FOCUS VICOBA kwa imani ya kwamba umeidhinishwa na Bunge.

Imetolewa na:
Idara ya Habari na Elimu kwa Umma,
Ofisi ya Bunge,
DODOMA                                                               Tarehe 15 Juni 2015

0 comments:

Post a Comment

SHARE