Pages

Ads 468x60px

Saturday, June 20, 2015

Njau Amjaribu Tena Tundu Lissu.......Atangaza Kugombea Tena Ubunge



MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) Taifa Wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Jonathan Njau, ametangaza kugombea kwa mara nyingine nafasi ya ubunge katika Jimbo la Singida Mashariki, baada ya mwaka 2010 kushindwa kufurukuta kwa Mbunge wa jimbo hilo, Tundu Lissu.
 
Katika uchaguzi huo wa mwaka 2010, Njau alishindwa kwa tofauti ya kura 1,626.
 
Mwanasheria huyo mkongwe, aliyasema hayo wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na mamia ya wana CCM.
 
Alidai kuwa safari hii amejipanga vizuri zaidi kushinda kwa kishindo nafasi hiyo.
 
Alisema ameamua kupeperusha tena bendera ya CCM kwenye kinyang’anyiro hicho baada ya kubaini kwamba kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, jimbo hilo limerudi nyuma kimaendeleo.

“Ndugu zangu wa Jimbo la Singida Mashariki, kila mmoja wenu ni shuhuda mzuri kwamba kuanzia Oktoba mwaka 2010 hadi sasa, jimbo letu limekuwa nyuma mno kimaendeleo katika sekta zote. Maendeleo pekee yaliyopatikana ni wananchi kuendelea kupotoshwa wasichangie wala kushiriki utekelezaji wa miradi yao ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa maabara,” alisema Njau ambaye hata baada ya kupinga matokeo hayo yaliyomwingiza madarakani Lissu alishindwa.

Akifafanua, Njau alisema wapotoshaji hao wakubwa kama wangekuwa wana mapenzi ya dhati na Jimbo la Singida Mashariki, wangekuwa hata na nyumba ya kuishi jimboni na sio kutegemea nyumba za kulala wageni.

“Nawaombeni wana CCM wenzangu na wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki, tuunganishe nguvu zetu pamoja ili Oktoba mwaka huu mnipe kura za kutosha, ili sote tushirikiane kuliendeleza jimbo letu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kile kijacho,” alisema Njau.

Kuhusu zoezi la uandikishaji kwenye daftari la wapiga kura, Njau amewataka wananchi wote wahakikishe wanajiandikisha ili kujijengea mazingira  mazuri ya kuchaguliwa na kuchagua viongozi bora kwenye uchaguzi mkuu.
 
“Mimi niwaombe tu ndugu zangu na hasa vijana, tuepukane na tabia ya kufuata mkumbo, kila mmoja wetu afanye maamuzi sahihi na sio maamuzi yanayotokana na kushawishiwa. Chagueni kiongozi ambaye hatatumia hila, ulaghai, upotoshaji na rushwa katika kujipatia kura, mkikubali kupotoshwa basi jimbo hili litaendelea kuwa la mwisho kimaendeleo kati ya majimbo yote hapa nchini,” alisema Njau.

0 comments:

Post a Comment

SHARE